‘WANAWAKE NA SAMIA’ 3000 MKOA WA DODOMA KUPATA MAFUNZO VETA
Na. Hellen M. Minja,
Habari – DODOMA RS
Chuo cha Mafunzo ya Ufundi Stadi(VETA) Mkoa wa Dodoma, kinatarajia kutoa mafunzo kwa kundi la ‘Wanawake na Samia’ wapatao 3000 linalounga mkono matamanio ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuleta Usawa wa kijamii na kijinsia ambayo ni kufikia mwaka 2030, ifike 50 kwa 50 kwa kila kundi kupata haki sawa.
Hayo yamesemwa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule alipokua akifungua mafunzo mbalimbali ya muda mfupi kwa ajili ya kundi la Wanawake na Samia Mkoa wa Dodoma, zitakazotolewa kwa kundi hilo na Chuo cha Mafunzo ya Ufundi Stadi (Veta) tawi la Jijini Dodoma.
“Mhe. Dkt Samia amekua akitamani kila kundi la Mtanzania lipate haki sawa ndio maana anasema hataachwa mtu nyuma awe ni mwanamke, mtu? mwenye ulemavu, mzee, kijana au mtoto. Anatamani Wanawake wa Tanzania washike uchumi sawa na wanaume, Makundi maalum ambayo yapo nyuma yashike uchumi sawa na makundi mengine”.
Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mhe. Jabir Shekimweri, amekipongeza Chuo cha VETA Dodoma kwa kuandaa mafunzo hayo ambayo kwa sehemu yake yatahusu utalii, ujasiriamali na maadili kwa kundi hilo ambalo linatunza heshima ya jina la Mhe. Dkt Samia na lipo Makao Makuu ya Nchi ambayo inazidi kukua na kujengeka.
Vilevile, Mkurugenzi Mkuu wa VETA CPA Anthony Mzee Kasore, amesema Chuo chake kinatoa mafunzo mbalimbali na eneo linalowekewa mkazo ni kuhakikisha wanawake wanaodahiliwa katika vyuo vya ufundi stadi wanaongezeka hadi kufikia 45% ambapo kwa sasa wapo asilimia 25 hadi 37 na wameanzisha programu za uwezeshaji wajasiriamali kwa akina mama ili kufikia lengo hilo.
Akizungumzia dhumuni la mafunzo hayo kwa kundi hilo, Mkuu wa VETA Dodoma Bw. Deodatus Orotha, amesema ni kuwapatia ujuzi wanawake wa Mkoa wa Dodoma ili waweze kutatua changamoto zao pamoja na familia lakini pia kuleta tija kwa Taifa. Amesema tayari wameshajisajili na mafunzo yataanza Machi 26, 2025 kwa muda wa wiki nne.
Nae, Mwenyekiti wa Wanawake na Samia Mkoa wa Dodoma Bi. Fatma Madidi amesema kuwa kundi lake linatoa shukrani kwa VETA kwa kukubali kutoa mafunzo hayo kwani kumsomesha mwanamke ni kuisomesha jamii na kupitia mafunzo hayo, watakwenda kutoa Wataalamu watakaosaidia Mkoa wa Dodoma, Tanzania na Dunia kwa ujumla.
Mafunzo hayo ambayo yatagharamiwa na VETA Dodoma, yanatarajiwa kuwanufaisha wanawake 3000 wa kundi hilo ambao watasoma kwa awamu ya wanawake 250 mpaka watakapokamilika ambapo wazo la kufanya mafunzo hayo lilitolewa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule
#dodomafahariyawatanzania
#keroyakowajibuwangu
#mtiwangubirthdayyangu
Comments
Post a Comment