"Sanaa na Utamaduni ni Ajira"- RC MTAKA


 Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Anthony  Mtaka ameeleza kuwa Sanaa, Utamaduni  na michezo ni fani zinazotoa ajira kwa vijana na kuchangia kwa kiasi kikubwa katika uchumi wa nchi.

Mhe. Mtaka amesema hayo Julai 23, 2022 Chamwino Dodoma wakati akifungua Tamasha la 13 la Muziki wa Cigogo linaloazimishwa kila mwaka.

"Nawaomba wazazi na walezi kuwaruhusu  vijana wenu  kushiriki shughuli za  Sanaa , utamaduni na michezo ni mojawapo ya ajira ambazo  zinachangia  katika pato la taifa"amesema Mhe. Mtaka

Aidha Mhe. Mtaka ametoa wito  kwa waandaaji wa  tamasha la Cigogo kuliongezea thamani tamasha hilo ili lifikie kiwango cha kitaifa na kimataifa kama lilivyo  tamasha la Sauti za Busara la Zanzibar.

Vilevile Mhe. Mtaka ametumia nafasi hiyo,kumpongeza Mwanzilishi wa Tamasha hilo Dkt. Kedmon Mapana kwa kuaminiwa na Mhe. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuteuliwa kuwa  Katibu Mtendaji wa Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) ambapo amemsihi kuendelea kukuza sanaa kwakua ni kazi ambayo anaijua vyema.

Pia Mhe. Mtaka amewataka wananchi kujitokeza kushiriki zoezi la Sensa Agosti 23,2022 ili kupata takwimu sahihi kwa maendeleo ya nchi.

Naye Mkurugenzi wa Maendeleo ya Sanaa Dkt. Emmanuel Ishengoma ameeleza kuwa dhamira ya   wizara hiyo ni kuhakikisha  inafanya mageuzi  ya Sanaa na Utamaduni kwa kuwa ni Sekta muhimu  zinazotoa ajira kwa vijana na kuchangia katika uchumi wa nchi.

Tamasha la Cigogo linafanyika kwa siku tatu  Julai 22 hadi 24,2022 likiongozwa na Kauli Mbiu "Elimu ya Sanaa ni Muhimu kwa Maendeleo Endelevu " linapambwa na ngoma mbalimbali za kitamaduni kutoka kabila la Wagogo Dodoma.


Mwisho






















Comments

Popular posts from this blog

WALIMU WATAKIWA KUFUNDISHA UZALENDO SHULENI.

TRAMPA KANDA YA KATI WAFANYA KIKAO DODOMA

BARAZA LA MITUME NA MANABII WAMTEMBELEA MKUU WA MKOA WA DODOMA