"WIZARA TAFUTENI SULUHU YA MBWA WOTE WANAOZURULA MITAANI "-MHE.SENYAMULE
“Kila mtu ambaye anafuga mbwa
lazima afuate sheria na taratibu zake, naagiza wataalamu wa mifugo wa Wizara na
Sekretarieti kutafuta suluhu ya mbwa wote wanaozurura mitaani. Mtu kama hawezi
kufuata sheria, aache kufuga wanyama hao” Amesema Mhe. Senyamule
Mkuu wa Mkoa ameeleza, ugonjwa
wa kichaa cha mbwa husababisha vifo 1500 kila mwaka nchini na Watoto chini ya
miaka mitano ndio wamekuwa wahanga wakubwa zaidi. Hivyo, Serikali inatekeleza
mpango mkakati wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi katika kutoa chanjo hii kila mwaka
ambapo mpaka sasa takribani mbwa 338,000 wameshachanjwa.
Mhe. Senyamule ametaja lengo la Dunia ni kutokomeza ugonjwa wa kichaa
cha mbwa ifikapo mwaka 2030 kwa kuhakikisha kuwa kila mbwa anapatiwa chanjo
kila mwaka. “Naomba utaratibu huu uwe endelevu mpaka ugonjwa huu uwe historia
kwani Tanzania bila kichaa cha mbwa, inawezekana. Tunatakiwa kuzingatia chanjo
pamoja na kupunguza idadi ya mbwa tunaofuga” Amesisitiza Mhe. Senyamule
Naye Mkurugenzi wa huduma za
mifugo Profesa Hezron Nonga, amesema nchini Tanzania tuna mbwa takribani
milioni 4.5 na paka milioni 2 wanaofugwa kwa malengo mbalimbali na kwa mwaka
kuna wastani wa matukio 2,030 ya mbwa wanaodhaniwa kuwa na kichaa. Hivyo
Shirika la Afya Dunia (WHO), Shirika la Afya za Wanyama duniani (WOAH) na
Shirika la chakula na kilimo (FAO) kwa pamoja wamekubaliana kutokomeza ugonjwa
wa kichaa cha mbwa ifikapo mwaka 2030.
“Takwimu zinaonyesha kuwa watu
zaidi ya 60,000 hupoteza Maisha kwa kichaa cha mbwa duniani kila mwaka. Kwa
Tanzania, kila mwaka wastani wa matukio ya majeraha kwa binadamu yanayotokana
na kuumwa na mbwa ni 3,387 na hiin ni kwa mujibu wa ripoti ya WHO ya mwaka
2017. Ugonjwa huu husababisha wastani wa
vifo vya binadamu 1500 kila mwaka” Prof. Nonga
Maadhimisho ya utoaji chanjo kwa
mbwa na paka hufanyika kila mwaka Duniani ikiwa ni kumuenzi muasisi wake Dr.
Luis Paster ambaye ndiye aligundua chanjo hii kwa wanadamu na mbwa kwa mara ya
kwanza mwaka 1885. Maadhimisho haya yanakwenda sambamba na utoaji wa chanjo
ambapo kwa mwaka huu chanjo zaidi ya
60,000 zenye thamani ya shilingi Milioni 180 zimetolewa, lengo ni kuchanja mbwa
kwa zaidi ya asilimia 70.
Aidha, maadhimisho ya mwaka huu yamebebwa na kauli mbiu inayosema, “Kichaa cha mbwa, afya moja, vifo sifuri” ikiwa na lengo la kutokomeza kabisa vifo vya binadamu vinavyotokana na ugonjwa wa kichaa cha mbwa.
MWISHO
Comments
Post a Comment