WATOTO 695,508 KUPATA CHANJO YA POLIO MKOANI DODOMA













Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma chini ya Idara ya Afya, imefanya kikao cha kamati ya afya msingi ikiwa ni katika kuhamasisha awamu ya nne ya utoaji wa chanjo ya kuzuia ugonjwa wa Polio kwa Watoto wenye umri kuanzia miaka 0 hadi miaka 5. Chanjo hiyo itaanza  kutolewa tarehe 1 Desemba mpaka 4, 2022.

Chanjo hii kama ilivyokua ikitolewa kwenye awamu zilizopita, inatarajiwa kutolewa nyumba kwa nyumba ili kuweza kufikia idadi kubwa ya Watoto wenye uhitaji wa huduma hiyo ambapo matarajio ni kuchanja Watoto 695,508.

Akihamasisha wazazi kushiriki kikamilifu kuwatoa Watoto wao wapate chanjo, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule amesema; “Dodoma tumefanya vizuri katika awamu zilizopita na leo tunajadili namna nzuri ya kwenda kutekeleza awamu hii ya nne.  Mhe.Rais ametimiza wajibu wake kwa kutoa fedha na sisi tutekeleze jukumu hili. Nasisitiza chanjo ni salama, wazazi andaeni Watoto wote. Ni imani yangu tutakwenda kutoa elimu tutakayoipata hapa kwa wazazi wenye Watoto wenye umri kuanzia miaka 0 hadi miaka 5. Wazazi mtafuatwa nyumba kwa nyumba Watoto wachanjwe, kwani Dodoma bila Polio inawezekana” RC Senyamule.

Kadhalika Katibu Tawala Mkoa wa Dodoma Dkt Fatma Mganga, amewaomba viongozi wa dini kuwatangazia waumini wote kuhakikisha Watoto wenye umri wa miaka 0-5 wanapata chanjo.Na kuwataka Wachanjani kufika maeneo ya ibada ambayo wazazi watakuwa pamoja na Watoto wao kwani tarehe 02/12 ni ijumaa na tarehe 04/12/2022 ni jumapili na wazazi wengi watakuwa maeneo ya ibada.

Aidha Dkt. Mganga ametoa shime kwa wachanjaji kuangalia muda mujarabu ambao wanaweza kuwakuta wazazi pamoja na watoto nyumbani kwani hivi karibu tunatarajia majira ya mvua na hivyo wazazi wengi watakuwa mashambani na Watoto wao.Hivyo ni vyema kwenda muda wa jioni ambapo watakuwa wametoka mashambani.“Tunatamani Watoto wetu wote wajitokeze ili tutokomeze Polio mkoa wa Dodoma” Dkt. Mganga

Vilevile, Afisa Afya Mkoa wa Dodoma anayesimamia zoezi hili Bw. Francis Bujiku, ametoa taarifa ya utoaji wa chanjo hii ya awamu ya nne.

“Awamu ya nne itafanyika kwa siku nne kuanzia Desemba 1 mpaka 4, 2022 ambapo zoezi hili litakwenda sambamba na utoaji wa huduma zingine ikiwemo elimu ya chanjo. Walengwa wa kampeni ya sasa ni Watoto 695,508. Kuna jumla ya chanjo 765, 059 zilizotolewa, huku bajeti ya utoaji chanjo hii kwa ngazi ya Mkoa ikiwa ni kiasi cha shilingi 45,524,000.00” Bw. Bujiku.

Ugonjwa wa Polio umekua tishio kwa miaka mingi katika nchi nyingi duniani ikiwemo Tanzania. Mara ya mwisho nchi yetu ilipata mgonjwa mwezi Julai mwaka 1996. Hivi karibuni nchi ya Malawi ilitoa taarifa ya mgonjwa wa Polio mnamo tarehe 17 Februari, 2022 katika mji wa Lilongwe hivyo Tanzania ilionekana ni miongoni mwa nchi zilizo katika hatari kubwa ya kupata maambukizi ya ugonjwa huu na ndio sababu Serikali kupitia Wizara ya Afya imefikia uamuzi wa kutoa chanjo hii kwa Watoto wote wenye umri wa miaka 0-5 nchini.

 

MWISHO

 

 

Comments

Popular posts from this blog

WALIMU WATAKIWA KUFUNDISHA UZALENDO SHULENI.

TRAMPA KANDA YA KATI WAFANYA KIKAO DODOMA

BARAZA LA MITUME NA MANABII WAMTEMBELEA MKUU WA MKOA WA DODOMA