MRADI WA REST WAZINDULIWA DODOMA


    
  








 

Mkoa wa Dodoma umezindua rasmi mradi unaoshughulikia masuala ya afya ya uzazi kwa vijana, wanawake na watoto unaojulikana kama Reproductive Equity Strategic (REST) unaoendeshwa na shirika lisilo la Kiserikali la Deutsche Shiftung Weltbevolkerung (DSW) - Tanzania ambao utafanya kazi kwenye Wilaya tatu za Mkoa ikiwa ni pamoja na Dodoma mjini, Bahi na Mpwapwa. Mradi huo umezinduliwa na Mkuu wa Mkoa Mhe. Rosemary Senyamule kwenye kikao kilichofanyika ukumbi wa jengo la Mkapa.

Akizindua mradi huo Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule amesema Serikali ya Awamu ya Sita imetoa kipaumbele katika sekta ya afya ikiwa ni pamoja na ujenzi wa miundombinu yake ili kuhakikisha wananchi wote wanapata huduma bora ya afya.

“Matokeo ya sensa ya mwaka 2022 yanaonyesha kuwa Tanzania ina jumla ya hospitali 676, vituo vya afya 1,466 na zahanati 7, 965. Tanzania Bara pekee ina hospitali 662, vituo vya afya 1,430 na zahanati 7,680 na mkoa wetu wa Dodoma una vituo vya afya 69 na zahanati 402. Hivyo ni muhimu sana kuendelea kuhamasisha wananchi hususan wakina mama wajawazito kutumia vituo vya afya kwa ajili ya kupata huduma, mpango wa Serikali ni kutokomeza vifo vya mama wajawazito na watoto wachanga ifikapo mwaka 2025” Amesema Mhe. Senyamule

Mheshimiwa Senyamule ametoa rai kwa waratibu na watekelezaji wa mradi huu kuweka malengo ya kufika kata nyingi zaidi za Mkoa wa Dodoma kwa lengo la kusogeza huduma kwa wananchi.

“Mradi huu unafanya kazi kwenye Kata 17 tu za Halmashauri hizi tatu, wakati Dodoma ina kata nyingi zaidi, tupange mkakati wa kuzifikia kata nyingi zaidi za mkoa ili muwe mfano wa kuigwa na kuvutia wengi zaidi kuwekeza Dodoma. Nitoe rai, mkafanye kazi kwa ufanisi mkubwa maana tunataka kila unachokifanya Dodoma, kifanyike kwa ufanisi kwani tunakwenda kuifaharisha Dodoma kwa mradi huu” Ameongeza Mhe. Senyamule

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Shirika la DSW Bw. Peter Owaga, amesema “mradi huu unatekelezwa kwenye mikoa minne ya Tanzania ambayo ni ambayo ni Arusha, Dar es Salaam, Dodoma, Mwanza na kwa mkoa wa Dodoma unatekelezwa katika Wilaya tatu ikiwemo Dodoma mjini, Bahi na Mpwapwa chini ya mashirika ya DOYODO, WOWAP na FAEAF wakiongozwa na Shirika la DSW Tanzania

Lengo la mradi huu ni kuwajengea uwezo asasi zisizo za kiserikali na kusaidia wanawake na wasichana wanapata na wanatumia huduma za afya ikiwemo afya ya uzazi ili kuleta ustawi wao na kuweza kutimiza matarajio na malengo ya maisha yao. Mradi huu pia utasaidia utekelezaji wa sera na miongozo mbalimbali ya afya ya uzazi ikiwemo kupinga unyanyasaji wa kijinsia na ukatili dhidi ya wanawake, wasichana na watoto.


MWISHO

Comments

Popular posts from this blog

WALIMU WATAKIWA KUFUNDISHA UZALENDO SHULENI.

TRAMPA KANDA YA KATI WAFANYA KIKAO DODOMA

BARAZA LA MITUME NA MANABII WAMTEMBELEA MKUU WA MKOA WA DODOMA