DUWASA YAJIPAMBANUA UHAKIKA WA MAJI DODOMA







Mamlaka ya maji safi na usafi wa Mazingira Mkoa wa Dodoma (DUWASA) inaendelea kufanikisha lengo la upatikanaji wa maji kwa asilimia 100 kwa Mkoa wa Dodoma kufuatia juhudi za Serikali ya awamu ya Sita. Hayo yamebainishwa wakati wa mfululizo wa vipindi maalumu vya kutangaza mafanikio ya Serikali kwa Taasisi za Umma vilivyoandaliwa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma ambapo leo kimeangazia sekta ya maji.

Akiwasilisha hotuba yake mbele ya wanahabari wakati wa utangulizi wa kipindi hicho, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule ameelezea miradi mbalimbali ya maji inayoendelea katika Mkoa na utekelezaji wake ndani ya kipindi hiki cha miaka miwili ya Serikali ya awamu ya sita.

“Tunafahamu maji ni kila kitu katika maisha ya mwanadamu, maji ni Uhai. Katika Mkoa wa Dodoma, kumekuwa na Uendelezaji wa vyanzo vya maji (uchimbaji wa visima na ujenzi wa mabwawa) kwa kutumia vyanzo vikuu kama vile Uchimbaji wa visima  virefu 34, Ujenzi wa Mabwawa 2 ya maji, miradi 10 ya maji inayotumia mtandao wa bomba imekamilika, Uzalishaji wa Maji umeongezeka kutoka wastani wa lita 61.5 Milioni hadi lita 67.8 Milioni. Ongezeko hili la uzalishaji limetokana na kukamilika kwa Miradi Mipya ya Maji yenye thamani ya Shilingi 9.14 Bilioni. Upatikanaji wa huduma ya Maji vijijini kwa Mkoa wa Dodoma umefikia wakazi 1,393,167 sawa na asilimia 65.1 na Lengo la Serikali ni kuhakikisha tunamtua Mama Ndoo kichwani miradi ya maji inaendelea kila Wilaya ili kufikia 85% ya upatikanaji wa maji vijijini ifikapo 2025” Amesema Mhe. Senyamule

Akifafanua mipango ya muda mrefu na wa kati ya Serikali kwa Mamlaka hiyo juu ya kuhakikisha upatikanaji wa maji unakua wa uhakika kwa Mkoa wa Dodoma, Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka hiyo Mhandisi. Aron Joseph amesema;

“Serikali ina mipango ya kati ya kuhakikisha inamaliza tatizo la upatikanaji wa maji ikiwemo mradi wa Bwawa la Farkwa katika Halmashauri ya Chemba unaogharimu kiasi cha Dola za Kimarekani Milioni 793.5, mradi wa kutoa maji kutoka Ziwa Victoria ambapo upo katika hatua ya usanifu. Pia kuna mpango wa dharura wa kuchukua maji kutoka Bwawa la Mtera lita Milioni 130 kwa siku sawa na asilimia moja ya maji yanayozalisha umeme ambayo yatasambazwa Dodoma nzima na mradi huu utagharimu kiasi cha Shilingi Bilioni 326” Amesema Mhandisi. Aron

Vilevile Mkurugenzi huyo ameainisha baadhi ya changamoto wanazokabiliana nazo katika utendaji wao wa kazi ikiwemo wizi wa miundombinu ya maji taka hasa mifuniko, wananchi kutupa taka ngumu kwenye mabomba ya maji taka hali inayopelekea mifereji kuziba na kusababisha kero ya kuvuja kwa maji taka kwenye makazi ya watu, wananchi kutozingatia matumizi sahihi ya maji safi hali inayopelekea upotevu wa maji, wanachi kutopenda kusoma taarifa za maji na kusababisha kero wakati wa kulipa bili, wizi wa maji pamoja na mita.

DUWASA ina matarajio makubwa kufikia mwaka 2025 ikiwemo kukamilika kwa miradi yote inayoendelea hivi sasa ili kutimiza lengo la Serikali ya Awamu ya sita kwa Makao makuu ya nchi kwani Serikali imehamia Dodoma na bado viongozi wanaendelea kuhamia kwa awamu tofauti hivyo ni lazima miundombinu ya maji iwe ya uhakika na thabiti ili kuweza pia kuvutia wageni wakiwemo wawekezaji wanaoingia kwa wingi katika Mkoa huu.

 

MWISHO

 

                                             

                                    

Comments

Popular posts from this blog

WALIMU WATAKIWA KUFUNDISHA UZALENDO SHULENI.

TRAMPA KANDA YA KATI WAFANYA KIKAO DODOMA

BARAZA LA MITUME NA MANABII WAMTEMBELEA MKUU WA MKOA WA DODOMA