DCT NA NEEMA YA MILLIONI 32.8 MWITIKILA-BAHI

















Vifaa vya Shule vyenye thamani ya Tsh.Millioni 32.8 vimekabidhiwa katika Shule za Msingi Mwitikira, Lupeta Mwitikira B na Shule ya Sekondari Mwitikira kwa ufadhili wa Kanisa la St. Pauls Richmond kutoka Marekani kwa kushirikiana na kanisa la Anglican Dayosisi ya Central Tanganyika (DCT), ambapo makabidhiano hayo yamefanyika April 17, 2024 katika viwanja vya kanisa la Anglican Parish ya Mwitikila Wilayani Bahi.

Vifaa hivyo ni madawati 290, meza 13, Viti 113  na Mashine ya kuchapia na kutolea kopi (printer machine) vimekabidhiwa na Askofu wa DCT Dickson Daud Chilongani kwa kaimu Mkuu wa Mkoa wa Dodoma  Mhe. Mayeka S. Mayeka ambaye amewakabidhi uongozi wa Halmashauri ya Bahi na Uongozi wa Shule hizo.

Akizungumza katika Hafla hiyo Mhe.Mayeka amewataka wakazi wa kata ya Mwitikira kuacha tabia ya kuwaachisha Watoto wao shule na kuwapeleka katika majiji mbalimbali kwa lengo la kufanya kazi za ndani zisizo na maslahi katika Maisha ya Watoto hao.

“Kuna mawakala wanaobeba Watoto vijijini  nikuombe OCD na timu yako tuwasake hawa mawakala ambao kazi yao ni kutembea kutafuta mabinti wawasafirishe kwenye miji mbalimbali kufanya kazi za ndani, hawa ni watu wabaya kabisa watoto wenu wanakumbana na unyanyasaji mkubwa wa kijinsia huko mnakowapeleka wakafanye kazi hawawezi kusema ni siri yao acheni mara moja tabia hii,” ameagiza Mayeka

Aidha Mhe. Mayeka amewaomba uongozi wa kanisa hilo kuendelea kuunga Mkono juhudi za Serikali kwa kutokukata tamaa ya kujitolea vitu mbalimbali ambavyo vinagusa Maisha ya Watanzania hususan katika Sekta ya Elimu.

Naye Askofu Chilongani ameahidi kuendelea kushirikiana na Serikali katika Sekta ya Elimu kwa kuweka bayana kuwa Kanisa hilo limewagharamia zaidi ya watu 7000 kwa ngazi zote za Elimu pasi na kubagua Imani za Dini za watu hao.

Hata hivyo Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashari ya Wilaya ya Bahi Bi. Zaina Mlawa amewapongeza DCT na kukiri kuwa misaada wanayoitoa imekuwa chachu ya kuongeza ufaulu kwa Shule za kata hiyo ikiwemo Shule ya Sekondari Mwitikila.



 

Comments

Popular posts from this blog

WALIMU WATAKIWA KUFUNDISHA UZALENDO SHULENI.

TRAMPA KANDA YA KATI WAFANYA KIKAO DODOMA

BARAZA LA MITUME NA MANABII WAMTEMBELEA MKUU WA MKOA WA DODOMA