RC ARIDHISHWA UTEKELEZWAJI WA MIRADI, ALIPONGEZA JIJI LA DODOMA.


 Septemba 11, 2024 Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule ametembelea na kukagua miradi ya Elimu na Afya inayotekelezwa katika kata nne (4) ambazo ni kata ya Zuzu, Nala, Kikuyu kaskazini na Tambukareli zinazopatikana katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

Akizungumza baada ya kumalizika kwa ziara hiyo RC Senyamule amewataka  uongozi wa Jiji la Dodoma kukamilisha miradi kwa wakati hususan miradi iliyotakiwa kukamilika katika kipindi cha mwaka wa fedha uliomalizika wa 2023/ 24 na kuwataka kukamilisha miradi hiyo Ifikapo Mwishoni mwa mwaka huu na wananchi waanze kupatiwa huduma.

‘’Mnapopata fedha za miradi mnatakiwa mzitoe mapema ili kuikamilisha miradi kwa wakati kwasababu kumekuwa na uchelewaji wa kutekeleza miradi kunakotokana na mwaka wa fedha kumalizika, hivyo nitoe wito kwa Jiji kuhakikisha miradi yote inakamilika na inaanza kutoa huduma kwa wananchi kwa muda uliokusudiwa.

Awali akizungumza katika mradi wa ujenzi wa kituo cha Afya Zuzu kinachotarajiwa kukamilika ifikapo Septemba 30, 2024  Senyamule ametoa maagizo kwa Halmashauri zote za Mkoa wa Dodoma kuhakikisha wanaanza mapema maandalizi ya kutumika kwa vituo vya afya kwa kufanya maandalizi yote Muhimu yanayohitajika.

‘’Tunafahamu tupo katika kampeni ya kupunguza vifo vya mama na mtoto na ujenzi wa vituo vya afya hivi ni katika kuweka huduma za afya karibu na wananchi ili kuepusha vifo vinavyoepukika vinavyotokana na umbali wa huduma hizo, nitoe maagizo kwa Halmashauri zote kuhakikisha wakati wanakamilisha ujenzi wa vituo vya afya pia endeleeni na mchakato wa kuanza manunuzi ya vifaa tiba na watoa huduma katika vituo hivyo ili vitakapokamilika tuu vianze kutoa huduma Mara moja’’.

Katika kuhakikisha na kuweka mazingira bora na ya kuvutia katika vituo vya afya na Hospitali za Mkoa wa Dodoma Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa Dkt. Nassoro Matuzya, amemuagiza Mganga Mkuu wa Jiji hilo pamoja na watumishi wote wa ofisi yake kupanda miti mine (4) kila mmoja na kuisimamia hadi itakapokua katika mradi wa Hospitali ya Wilaya hiyo inayojengwa katika kata ya Nala.

 Hatahivyo Mhe. Senyamule amewapongeza Jiji hilo kwa Usimamizi mzuri wa miradi pamoja kutekeleza miradi mbalimbali kupitia mapato ya ndani ikiwa ni sehemu ya kurudisha kwa kwa jamii (SCR) hali inayochangia mahusiano mazuri kwa Jamii inayowazunguka.

Katika ziara hiyo amekagua ujenzi wa miradi ya Kituo cha Afya Zuzu unaogharimu Tsh. 259,000,000, Ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Dodoma Unaogharimu Tsh. Billioni 1.5, Ujenzi wa Vyumba 2 vya madarasa na Matundu 8 ya vyoo katika Shule za Sekondari Kikuyu na Sechelela Unaogharimu Milioni Tsh 120,800,000 @ 60,400,000 ambapo ujenzi wa Miradi yote upo katika hatua ya Umaliziaji.

 

 

Comments

Popular posts from this blog

WALIMU WATAKIWA KUFUNDISHA UZALENDO SHULENI.

TRAMPA KANDA YA KATI WAFANYA KIKAO DODOMA

BARAZA LA MITUME NA MANABII WAMTEMBELEA MKUU WA MKOA WA DODOMA