DODOMA YAMALIZA MBIO ZA MWENGE WA UHURU 2025 NA KUUKABIDHI IRINGA
Na. Hellen M. Minja
Habari – DODOMA RS
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule, leo Aprili 28, 2025 amekabidhi Mwenge wa Uhuru 2025 rasmi kwa Mkuu wa Mkoa wa Iringa Mhe. Peter Serukamba baada ya kukimbizwa kwa KM 1333 kwenye Wilaya zote saba (7) na Halmashauri nane (8) za Mkoa huu kuanzia Aprili 20 hadi 27 ulipokamilisha Mbio zake.
Akizungumza na hadhara iliyojitokeza katika makabidhiano hayo yaliyofanyika kwenye Kijiji cha Makatapora Wilaya ya Iringa, Mhe. Senyamule amesema miradi yote iliyochaguliwa imepitiwa na Mwenge huo.
“Katika Mkoa wetu, Mwenge wa Uhuru umeweza kutembelea miradi 56 yenye thamani ya Shilingi Bilioni 61.1 Nami nakiri kwa kusema, katika Mkoa wa Dodoma miradi yote imepitiwa, kukaguliwa, kuwekewa mawe ya msingi, kutembelewa na tumepata ‘clean sheet’.”
Mhe. Senyamule ameongeza kuwa, wakati wa mbio hizo Mkoani hapa, wameweza kufanya mazoezi ya kupima Virusi vya Ukimwi, kuchangia damu na magonjwa mengine na yote yamedhihirisha kuwa, Dodoma kwenye Malaria ipo vizuri, maambukizi ya Ukimwi yapo chini na maelekezo yote yaliyotolewa na Kingozi wa mbio hizo yanafanyiwa kazi.
Kadhalika, kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru 2025 Kitaifa ndugu Ismail Ali Ussi, ametaja mambo muhimu ya kuzingatia kwa Mkuu wa Mkoa wa Iringa Mhe. Peter Serukamba pindi Mwenge utakapokua unapita kwenye maeneo ya miradi ndani ya Mkoa wake.
“Halmashauri na Wilaya zote ziandae taarifa za miradi ambazo tutaziweka kwenye magari yetu na wakufunzi, waandae vifaa vyote ambavyo vitatumika kupimia ubora wa miradi ambayo tutapitia ili iweze kutuonesha kama ni ya kukagua, kuzindua ama kuweka mawe ya msingi, nyaraka, taarifa na wataalamu tuwakute katika maeneo yote”. Ndugu Ismail Ussi.
#dodomafahariyawatanzania
#keroyakowajibuwangu
#mtiwangubirthdayyangu
#kwaherimwengewauhuru2025mkoawadodoma
Comments
Post a Comment